Ubalozi wa Tanzania Visiwani Comoro kwa kushirikiana na Umoja na Vijana Visiwani hapa ujilikanao kama Udjamaa wa Komori na Afrika Mashariki tarehe 13 Oktoba, 2018 uliadhimisha siku ya Mwalimu Nyerere (Nyerere Day). Maadhimisho hayo yalifanyika katika ukumbi wa mkutano wa Ubalozi uliopo katika mtaa wa Oasis, Moroni, Visiwani Comoro.

Hii ni mara ya kwanza kufanyika maadhimisho hayo Visiwani hapa ambapo lengo lake ilikuwa ni:-

Kuonyesha mchango wa Mwalimu Nyerere na Tanzania kwa ujumla katika ukombozi wa Visiwa vya Comoro.
Kuelezea historia ya baba wa Taifa hasa kwa Vijana wa Comoro amabapo historia hiyo ilipotea kutokana na juhudi za Mfaransa.
Kudumisha ushirikiano wa kihistoria na kindugu uliopo baina ya Tanzania na Comoro hasa kwa kuzingatia kwamba Comoro ipo katika harakati za kujianga kwenye Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Katika maadhimisho hayo, Balozi wa Tanzania, Visiwani Comoro, Mhe. Sylvester M. Mabumba alifanya mahojiano na vyombo mbalimbali vya habari viliopo Visiwani hapa na kuelezea kuhusu maisha na Mwalimu Nyerere na mchango wake katika harakati za ukombozi kwa Bara la Afrika. Aidha, katika hilo Mhe. Balozi alisistiza kudumisha amani Visiwani Comoro wakati nchi hiyo ikielekea kwenye uchaguzi Mkuu wa Rais mapema mwaka 2019.